Thursday, August 9, 2012

Basi la Sabena laua 17, lajeruhi 78, lilibeba zaidi ya abiria 100

Basi la Sabena baada ya ajali ilyoua watu 17 jana
 Sikukuu ya Wakulima na Wafugaji (Nane Nane), iliyoadhimishwa kote nchini jana, imeacha kilio baada ya ajali ya basi kukatisha uhai wa watu 17 na wengine 78 kujeruhiwa wilayani Sikonge katika Mkoa wa Tabora.
Ajali hiyo ilitokea katika eneo la Kitunda wilayani Sikonge umbali wa kilometa 200 kusini mwa mji wa Tabora, likihusisha basi la Sabena, aina ya Scania lenye namba T570 AAM, ambalo lilipinduka likiwa safarini kutoka Tabora kwenda mkoani Mbeya.
Watu wanne kati ya majeruhi 78, wamejeruhiwa vibaya na kulazwa katika Kituo cha Afya cha Kitunda huku mipango ilikuwa ikifanywa kuwahamishia Hospitali ya Mkoa, Kitete kwa huduma zaidi.
Abiria wengine 54 waliokuwa katika basi hilo, walinusurika na kuomba kuendelea na safari, baada ya kufanyiwa uchunguzi na kugundulika kuwa hawakuwa na madhara makubwa katika miili yao.
Miongoni wa watu walikufa ni watoto watano, wanawake sita na wanaume sita ambao miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Kitete kwa ajili ya kutambuliwa na ndugu na jamaa zao.
bonyeza chini kuendelea kusoma zaidi na more pictures



Kamanda wa Polisi mkoa wa Tabora, ACP Antony Rutta akitoa maelezo ya ajali kwenye eneo la tukio kwa waandishi wa habari
Hata hivyo, hadi kufikia jana mchana, miili ya watu saba ilikuwa imetambuliwa na baadhi ya ndugu ukiwamo mwili wa askari Polisi, Konstebo Kheri wa Kituo Kikuu Kikuu cha Polisi mjini Tabora.
Wengine ni Vitus Tulumanye ambaye ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (SAUT), Tawi la Tabora na Farah Inga ambaye ni raia wa Zimbabwe aliyekuwa akifanya kazi Tabora.
Pia wamo Ikamba Thadeo, Damalu Goma, Beatrice Kalinga ambaye ni Mwalimu wa Shule ya Msingi Igoko wilayani Uyui na Andrew Madirisha ambaye ni mwalimu wa shule ya msingi katika wilaya mpya ya Kaliua.
Mwalimu Madirisha anadaiwa kufuatana na watoto wanne na mkewe ambaye hajatambuliwa na kwamba juhudi za kuhakikisha kama hiyo ni familia ya Mwalimu huyo ama la, ili kuifahamisha jamii.
Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na dereva wa basi hilo aliyenusurika kifo, chanzo ni lori aina ya Fuso lililokuwa limeegeshwa katika kona, hivyo alipojaribu kulikwepa, mtarimbo wa usukani ulikatika na hivyo gari kuacha njia na kupinduka.
Dereva huyo, Ali Nassoro alibaini kwamba ajali hiyo ilitokea saa sita na nusu mchana juzi ambapo eneo walilopata ajali halina mawasiliano ya simu za mkononi na hata kwenye kijiji cha Kitunda, hivyo kushindwa kulipoti ajali hadi walipopata mtu aliyekwenda Sikonge kutoa taarifa.

 

Joyce Mwasilombe, abiria aliyesalimika akiwa na mwanae akielezea juu ya ajali hiyo

Baadhi ya majeruhi wametambuliwa kwa majina ya Grace Mbunga, Kayungilo Nsungu, Zena Shigela, Ndisi Ngosha, Kulwa Kija, Feni Salum, Shinje Kayogole na Emmanuel Charles.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Antony Ruta, alithibitisha kutokea kwa ajali na kuwataka abiria wanaotumia usafiri wa mabasi kutoa taarifa mara baada ya kuona basi ambalo wanasafiri nalo limejaa kupita kiasi kwani basi hilo lilikuwa na abiria zaidi ya 100.
Hata hivyo, askari wa Jeshi, Shabani Mtawazi alirushia lawama Jeshi la Polisi hasa Kikosi cha Usalama Barabarani, akisema tangu wanaondoka mjini Tabora, wamekuwa kukikaguliwa na trafiki na kutoa malalamiko yao, lakini hakuna hatua zozote zilichukuliwa na askari hao.
Mwanajeshi huyo aliyenusurika kifo alisema dereva wa basi hilo alikuwa mwendo kasi na kuwalalamikia askari hao, lakini waliweka pamba masikioni na kusababisha hali hiyo ya vifo iliyotokea.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Kurda Mwinyimvua alikwenda eneo la ajali akifuatana na uongozi wa Hospitali ya Mkoa kupeleka wauguzi zaidi na dawa kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu walionusurika.

No comments:

Post a Comment