Friday, March 16, 2012

MSANII WA BONGO MOVIE KAJALA MASANJA APANDISHWA KIZIMBANI

Msanii wa Bongo movie Kajala akiwa anatoka eneo la mahakama jana
 
Msanii wa Bongo Movie, anayekuja juu kwenye tasnia ya filamu Tanzania na ambaye pia amewahi kucheza movies kadhaa ikiwemo ya Devil’s Kingdom sambamba na Steven Kanumba na Ramsey Noah wa Nigeria, Kajala Masanja amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa mashitaka matatu yakiwamo ya kutakatisha fedha haramu kosa ambalo halina dhamana kisheria na hivyo kurudishwa lupango.

Kajala akiwa pamoja na Ramsey Noah katika shooting ya movie ya Devils Kingdom

Katika kesi hiyo, Kajala anashitakiwa pamoja na mumewe Faraji Mchambo ambapo makosa mengine ni kula njama na kubadilisha umiliki wa nyumba.
  
Wakili wa serikali Leonard Shayo mbele ya Hakimu Mkazi Sundi Fimbo alidai kuwa Kajala na mumewe wameshitakiwa kwa kosa la kwanza la kula njama kinyume na kifungu cha 34 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007 ambapo washtakiwa wote walitenda kosa hilo la kuhamisha umiliki wa nyumba iliyopo Kunduchi Salasala jijini Dar es Salaam.


Shtaka la pili walidaiwa kuwa mnamo Aprili 14 2010 walihamisha umiliki wa nyumba hiyo kinyume na kifungu cha 34(2)A(3) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007.

Ambapo shtaka la tatu walidaiwa Aprili 14 2010 huku wakijua ni kinyume na sheria walifanya kosa la kutakatisha fedha haram ambapo ni kosa lisilo na dhamana kisheria.

Kajala akiwa katika pozi
Chambo hakuwepo mahakamani kwasababu yupo gerezani mahabusu kwa makosa mengine ambayo hayana dhamana yanayomkabili ya utakatishaji fedha.


Kajala alikana mashtaka hayo na kurudishwa rumande kwa uchungu mkubwa huku akilia pamoja na ndugu zake akiwamo mama yake aliyekuwepo mahakamani hapo.

Hakimu Fimbo aliarisha kesi hiyo mpaka Aprili 20 mwaka huu ili kesi ije kwaajili ya kutajwa na pia kutolea maamuzi, maombi yaliyotolewa na wakili wa Alex Mgongolwa anayemtetea kajala.

No comments:

Post a Comment