Friday, June 29, 2012

WAZO LA LEO: NI UTAMADUNI TULIOJICHAGULIA


Watanzania wengi bado hatujaweza kutambua uwezo mkubwa tuliokuwa nao katika kuchangia maendeleo yetu. Inaeleweka kwamba kumekuwa na kilio kikubwa kuhusu michango ya kila siku katika sekta ya elimu. Hatahivyo mengi ya malalamiko haya yanatokana zaidi na wasiwasi wa matumizi ya michango husika. Michango hii ikielekezwa mahala stahiki na kuhusisha wachangiaji juu ya matumizi yake ina uwezo mkubwa sana wa kubadilisha maisha ya watoto wetu walioko mashuleni.Tatizo sio UWEZO, tatizo hasa ni NIA.
Watanzania kwa kiasi kikubwa tumekuwa na utamaduni wa kuchangia zaidi shughuli zinazoshahabiana na anasa kuliko kuchangia maendeleo. Kwa wenzetu wakenya kuchangia watoto wa majirani kwenda shule ni sehemu ya utamaduni uliojikita. Mathalani kwa mkoa wa Dar es Salaam ambapo kuna watanzania zaidi ya milioni nne watu 100,000 huudhuria sherehe za harusi kwa mwezi kiwango cha chini cha uchangiaji kawaida ni Tshs 60,000. Kama hii ndiyo hali inamaanisha kuwa kwa mwaka sisi wakazi wa Dar es Salaam tunatumia kiasi cha shillingi 72,000,000,000,000 kiasi ambacho kingeweza kupeleka watoto 720,000 kwa gharama ya Shillingi 100,000 kwa mwaka. Kwahiyo tungetoa asilimia kumi tu ya matumizi yetu kwenye harusi tungepeleka watoto 72,000 shule kila mwaka!!!Labda tutaulumu mfumo wetu wa ujamaa kwa kutuzoesha kwamba tungeweza kupata huduma zote toka serikalini. Serikali ikawa ndio baba ndio mama na hivyo hata wajibu wa kimsingi kama kupata elimu ya msingi tukaiachia serikali. Umiliki wetu wa jambo hili la msingi na lazima ukapotea kwa utaratibu huo.
Ni rahisi kusema kuwa serikali inakusanya kodi kwahiyo ifanye kila kitu lakini ni sawa na kuomba rafiki yako amtunze mwanao wakati ukilipia gharama za matunzo hayo. Ni dhahiri bado utahitaji kuingia gharama za kuhakikisha mwanao anapata matunzo yanayokidhi mahitaji na ndipo hapo kila mara utakapomtembelea mwanao utajikuta ukiongeza kagharama kidogo ka kununua pipi, kubadili nepi, kubadili maziwa na vitu vingine vidogo vidogo ambavyo huwa haviachi kuibuka. Bila shaka wote tukichulia elimu kwa uzito tunaouchukulia watoto wetu wa kuzaa tunaweza kupiga hatua.Natoa wito kwa kila mmoja wetu kutafakari nafasi yake katika maendeleo ya elimu nchini. Tunaweza kuendelea kukaa kimya au kuchukua hatua sasa. Nwakaribisha vile vile kuendeleza mjadala kupitia ukurasa wa faceboo @Educate the Children of Tanzania na kupitia twitter @shujaawakarne.Mwandishi wa makala haya ni Katibu Mtendaji wa asasi ya EDUCATE THE CHILDREN; asasi ya kitanzania inayojihusisha na kuchochea upatikanaji wa elimu bora kwa watoto wa kitanzania na kwa namna ya pekee watoto wanaotoka kwenye familia duni.

No comments:

Post a Comment